FISI WASHAMBULIA MIFUGO MGOLOLO

 

Wananchi Wilayani Mufindi wametakiwa kutoa ushirikiano wa kumsaka fisi ambaye ameua mifugo aina ya Nguruwe wawili kondoo Wanne na kujeruhi kuku katika bonde la Mgololo usiku wa Julai 03 mwaka huu.



Akitoa ufafanuzi wa sintofahamu iliyozuka katika kata ya Makungu, Afisa Habari na Mawasiliano Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Bw. Ndimyake Mwakapiso, amesema baada ya taharuki kuwakumba wananchi wa Kijiji cha Mabaoni na kitongoji cha Lole wakihofia kuwa ni Simba, uchunguzi uliyofanywa na Afisa Wanyamapori umebaini kuwa ni Fisi.

Aidha Bw. Mwakapiso, amewataka wananchi kuishi kwa tahadhari wakati juhudi za kumtafuta na kumuuwa mnyama huyo zikiendelea.

Awali Kaimu Mwenyekiti wa kamati ya Ulinzi na Usalama Kijiji Cha Mabaoni Ndg Thobias Jonas Mkwama, amethibitisha kupata taarifa hizo asubuhi toka kwa mmiliki wa Mifugo Ndg Amlike, na hatua zikachukuliwa .

Mmiliki wa Nguruwe Ndg Amlike, amesema ilikua asubuhi akipeleka chakula kwenye banda wanaloishi wanyama hao, ndipo alipobaini kuwa Nguruwe wawili hawamo bandani na kuwepo kwa alama za damu pamoja na vipande vya nyama vikiwa vimeachwa nje ya banda Hilo.

Hata hivyo, Mkuu wa hifadhi ya Taifa ya Ruaha, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Godwell Ole Meingataki, amesema Simba waliokadiriwa kuwa watano, waligawanyika katika makundi mawili, moja limerudi hifadhini na lingine lipo katika Kijiji cha Isingo karibu na mashamba ya mwekezaji (hakutajwa jina) ambako kuna msitu mnene.

Post a Comment

0 Comments